Waziri MKuu wa Ugiriki Alexis
Tsipras amewaomba wapiga kura kupinga vitisho na kusema 'La' wakati wa
kura ya maamuzi ya hapo Jumapili.
Katika hotuba fupi kwenye
runinga ya taifa, Bw Tsipras amesisitiza kwamba hakuna tisho lolote la
Ugiriki kufukuzwa kutoka Muungano wa Ulaya.Amewaambia wafuasi wake kupuuza kelele za wale aliowataja kama wanaotoa vitisho.
Hapo Jumapili wapiga kura wa Ugiriki wataamua kuunga au kukataa masharti ya kupokea mkopo kutoka kwa mashirika ya kimataifa.Ugiriki ilishindwa kuafikiana na wakopeshaji wake wakati wa mazungumzo ya miezi kadhaa.Viongozi wa Ulaya wameonya kwamba kura ya 'La' huenda ikasababisha Ugiriki kuondoka kanda inayotumia sarafu ya Euro.
Kwa sasa uchumi wa Ugiriki unakumbwa na msukosuko mkubwa baada ya nchi hiyo kushindwa kupata mkopo wa dharura.Benki za nchi zimefungwa huku kukiwekwa kiwango rasmi ambacho wateja wanafaa kutoa.
Hakujafanyika mihadhara, mikubwa mjini Athens lakini mabango ya 'La' na 'Ndio' yametawala kote mjini Athens kila upande ukijaribu kuwashawishi wapiga kura.
"MSUKOSUKO WA UCHUMI UGIRIKI UMECHUKUA SURA MPYA"